Nguzo Za Swalah, Vitendo Vya Waajib Na Sunnah Katika
Swalah
imekusanywa na Abubakari shabani Rukonkwa.
imerejewa na Ummu Rahma
Swalah
Nguzo za Swalah ni 14: Nguzo ni zile ambazo ukiswali na
ukaziacha kwa makusudi Swalah yako inabatilika, na ikiwa
umeacha kwa kusahau, Swalah yako pia itakuwa haikukamilika
hadi urejee kitendo chenyewe au urejee rakaa na kisha
mwishoni utoe Sajdatus-Sahw. Lakini ukiwa umesahau nguzo
ya Takbiyratul-Ihraam, basi itakubidi uiswali Swalah upya tokea
mwanzo.
Nguzo hizo 14 ni hizi zifuatazo:
1. Kusimama katika Swalah za Fardh kwa yule mwenye uwezo.
(Wanachuoni wengine wamesema nguzo ya kwanza ni Niyah
kabla ya Kusimama). Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema:
"Na simameni kwa ajili ya Allaah hali ya kuwa watiifu" (Al-
Baqarah: 238).
Na Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)
amesema: "Swali hali ya kuwa umesimama, usipoweza, basi
kwa kukaa na usipoweza basi kwa kulala ubavu" (Al-Bukhaariy
na Abu Daawuud).
2. Takbira ya kuhirimia (Takbiyratul-Ihraam) kwa tamko la
Allaahu Akbar kutokana na kauli ya Mtume (Swalla Allaahu
'alayhi wa aalihi wa sallam): "Ufunguo wa Swalah ni
kujitwaharisha, na kuifunga ni Takbira, na kuifungua ni kutoa
Salaam" (Abu Daawuud na At-Tirmidhiy).
3. Kusoma Suratul-Faatihah katika kila rakaa. Mtume (Swalla
Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) anasema: "Hapana Swalah
kwa ambaye hakusoma Suratul Faatihah" (Al-Bukhaariy).
4. Kurukuu.
5. Utulivu (Twumaaniynah) katika Rukuu.
6. I'itidaal (hapa inaingia na kunyanyuka kutoka katika Rukuu
hadi anaponyooka mtu).
7. Utulivu katika I'Itidaal.
8. Kusujudu.
9. Utulivu katika kusujudu. Kutulia wakati wa kurukuu,
kusujudu, kusimama, kukaa baina ya Sijdah mbili kwa msemo
wa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): "Kisha
rukuu mpaka utulizane hali ya kurukuu, kisha nyanyuka mpaka
ulingane sawa hali ya kusimama, kisha sujudu mpaka utulizane
na hali umesujudu, kisha nyanyuka mpaka utulizane hali ya
kuwa umekaa" (Al-Bukhaariy).
10. Kikao baina ya Sijda mbili.
11. Utulivu katika kikao baina ya Sijda mbili.
12. Tashahhud ya mwisho.
13. Kikao katika Tashahhud ya mwisho.
14. Salaam (Kutoa Salaam) ya kwanza.
Utahakikisha unafuatanisha yote hayo kama utaratibu
ulivyopangika.
Waajib Za Swalah(VIPASAJI)
Ni lile ambalo ni wajibu kulifanya au kusema, inaondoka kwa
kusahau na kulazimisha mwenye kuswali kusujudu sijdah mbili
za kusahau. Yeyote mwenye kuacha kwa kusudi Swalah yake
inabatilika ikiwa anajua uwajibu wake.
Istilahi hii inatumika kwa madhehebu ya Hanafi na Hanbali ila
ma-Hanafi hawaoni kuwa mwenye kuacha wajibu kwa kusudi
inabatilisha Swala yake bali yeye amefanya madhambi
anayostahiki adhabu. Ama ma-Maaliki na ma-Shaafi'y hawana
kigawanyo hichi cha Waajib kwao ila wao wana nguzo na
Sunnah kwa ujumla wake.
Ama hapa tutaweka yale yaliyotajwa ambayo yanaelekea kuwa
na nguvu zaidi.
Kwanza kabla hatujataja mambo yenyewe, tunapaswa kujua
kuwa mambo ya Waajib ni yale ambayo vilevile atakapoacha
mtu kwa makusudi hubatilika Swalah yake, na atakapoacha kwa
kusahau inamtosheleza yeye kusujudu Sijda mbili za kusahau
'Sujuudus-Sahw'.
Ama mambo ya Waajib ambayo yametajwa katika kitabu cha
'Swahiyhu Fiqhus-Sunnah' kwa dalili mbalimbali za Aayah na
Hadiyth ni 9 kama yafuatayo:
Du'aa ya ufunguzi wa Swalah 'Du'aa al-Istiftaah'.
Kusema 'A'udhu biLlaahi Minash-Shaytwaan ar-Rajiym' kabla
ya kusoma 'BismiLlaah ar-Ramaanir Rahiym' na 'Suratul-
Faatihah'.
Kusema 'Aamiyn' baada ya Suratul-Faatihah.
Takbiyrah za kuhama baina ya kitendo na kitendo.
Kusema 'Sami'aLlaahu liman hamidah'Kusema 'Rabbana Lakal
Hamdu' katika I'itidaal.Kusema 'Subhaana Rabbiyal 'Adhwiym'
wakati wa kurukuu na kusema 'Subhaana Rabbiyal A'ala' wakati
wa kusujudu.Tashahhud ya kwanza.Kikao cha Tashahhud ya
kwanza.
Wanachuoni wengine wametaja mambo ya Waajib ni 8 kama
yafuatayo:
Takbiyrah nyingine zote isiyo ile ya Ihraam.Kusema
'Sami'aLlaahu liman hamidah' kwa Imaam na mwenye kuswali
peke.
Kusema 'Rabbana Lakal Hamdu'.Kusema 'Subhaana Rabbiyal
'Adhwiym’ mara moja kwenye kurukuu.
Kusema 'Subhaana Rabbiyal A'ala' kwenye kusujudu.
Kusema 'Rabbi-Ghfir liy' kwenye kikao baina ta Sijda mbili.
Tashahhud ya mwanzo.Kikao katika Tashahhud ya
mwanzo.Hizi ndizo maarufu zaidi kwa wanachuoni wengine.
Sunnah Za Swalah
Hizi ni kauli na vitendo zinazopendeza kuletwa katika Swalah.
Mwenye kufanya hayo hupata thawabu wala Swalah haibatiliki
kwa kuachwa hata kwa kusudi. Wala sijdah ya kusahau hailetwi.
Hapa tuna vigawanyo viwili vya Sunnah katika Swalah; Sunnah
za kauli na Sunnah za vitendo.
Sunnah Za Kauli
Kisomo baada ya al-Faatihah.Dhikr nyinginezo katika Rukuu.
Dhikr baada ya kusimama kutoka katika Rukuu na baada ya
kusema ‘Rabbana Lakal Hamd’.Dhikr nyinginezo katika
Sujuud.Du’aa baina ya Sijdah mbili.Kumswalia Mtume (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) katika Tashahhud ya
kwanza na ya pili.Du’aa baada ya Tashahhud ya kwanza na ya
pili.Salaam ya pili.
Dhikr na du’aa mbalimbali baada ya Swalah.
Sunnah Za Vitendo
Kuweka Sutrah (kizuizi mbele ya sehemu unayoswalia) katika
Swalah.
Kunyanyua mikono wakati wa Takbiyratul Ihraam, na wakati
wa kurukuu na na wakayi wa kunyanyuka kwayo na wakati wa
kuinuka kutoka katika Tashahhud ya kwanza. Na kadhalika
wakati unapoinama na kuinuka.Kuweka mkono wa kuume juu
ya mkono wa kushoto juu ya kifua unaposimama kuswali.
Kutazama mahali pa kusujudu.
Kulingana sawa mgongo unaporukuu na kutonyanyua kichwa au
kukiinamisha sana, na kuweka viganja kwenye magoti mawili
na huku umeviachanisha vidole vya mikono na kuachanisha
viwiko visiguse mbavu au tumbo lako.
Kuteremka katika Sijdah kwa mikono miwili kabla ya magoti
(Wengine huona kushuka kwa magoti kabla ya mikono).
Kuimakinisha paji la uso, pua na mikono (viganja viwili)
kwenye ardhi pamoja na kupanua mikono isiguse mbavu zako;
kuwe na uwazi wa kuweza kupita kinyama kidogo. Na viganja
vyako viwe usawa wa mabega au masikio wakati uko katika
kusujudu na viwiko vikiwa vimenyanyuliwa juu na vidole vya
mikono vikiwa vinaelekea Qiblah. Matumbo ya vidole vya
miguu yakiwa ardhini visigino vikielekea juu na hali vidole vya
miguu vikielekea Qiblah.Kulilalisha guu la kushoto na
kulisimamisha la kulia wakati wa kikao baina Sijdah mbili.
Kurefusha kikao baina ya Sijdah mbili.Kikao cha mapumziko
baada ya kukamilisha rakaa ya kwanza na ya tatu.Kutegemea
ardhi kwa mikono wakati mtu anaponyanyuka kutoka kusujudu
na kwenda kwenye rakaa nyingine.
Kukaa kikao cha Iftiraash (Kusimamisha mguu wa kulia na
kukalia mguu wa kushoto) katika Tashahhud ya mwanzo. Na
kukaa kikao cha Tawarruk (kusimamisha mguu wa kulia na
kuipitisha mguu wa kushoto chini ya muundi wa mguu wa kulia
na huku kikalio chako kimekaa juu ya ardhi).
Kuashiria kwa kidole cha shahada katika Tashahhud kuanzia
mwanzo hadi mwisho bila kukishusha na huku unasoma na
ukikitazama.
(Abu Maalik Kamaal Saalim, Swahiyh Fiqhus Sunnah, Mj. 1).
Hata hivyo, Shaykh Abu Bakar Jaabir al-Jazaairiy katika kitabu
chake Minhaajul Muslim yeye amegawanya Sunnah za Swalah
katika mafungu mawili: Zilizotiliwa mkazo kama vile Waajib na
zisizotiliwa mkazo.
Sunnah Zilizotiliwa Mkazo
Kusoma Surah au Aayah katika Qur-aan baada ya Suratul
Faatihah katika Swalah ya Asubuhi, rakaa mbili za mwanzo za
Swalah ya Adhuhuri, Alasiri, Maghrib na 'Ishaa.
Kusema ‘Sami'a Alaahu liman Hamidah’ wakati wa kuitadili na
kisha Rabbaana walakal Hamd, Subhaana Rabiyal 'Adhiym
wakati wa kurukuu, Subhaana Rabiyal A'alaa wakati wa
kusujudu.
Takbira ya kuhama.
Tashahhud ya kwanza na tamko lake.Kusoma kwa uwazi katika
Swalah ya kusoma kwa uwazi na kusoma kwa siri katika Swalah
ya kusoma kwa siri.Kumswalia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi
wa aalihi wa sallam) katika Tashahhud ya mwisho.
Sunnah Zisizotiliwa Mkazo
1. Du'aa ya ufunguzi.
2. Kusoma A’udhubiLlaah.
3. Kunyanyua mikono miwili mpaka usawa wa mabega.
4. Kusema Aamiyn.
5. Kurefusha kisomo katika Swalah ya Asubuhi na kupunguza
katika Swalah ya Alasiri na Maghribi.
6. Namna ya mkao, nayo ni kukalia mguu katika vikao vyote na
kukalia tako katika kikao cha mwisho. Mikao ni wa Iftiraash
(kukalia tumbo la mguu wa kushoto na kuunyoosha unyayo wa
mguu wa kulia) na Tawarruk (kuweka tumbo la mguu wa
kushoto chini ya paja la kulia na kuweka kikalio ardhini na
kunyoosha unyayo wa mguu wa kulia).
7. Kuweka mikono juu ya kifua, wa kulia juu ya wa kushoto.
8. Du'aa katika Sijdah.
9. Du'aa katika Tahiyyaatu.
10. Kuanzia kulia kutoa salaam.
11. Kutoa salaam ya upande wa kushoto.
Ingawa kuna ikhtiliaaf ya hao wanachuoni, tunapenda
kuwakumbushia Hadiyth ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa
aalihi wa sallam)aliyesema: "Swalini kama mlivyoniona
nikiswali" (Al-Bukhaariy).
Kwa hivyo, ni juu yetu kufanya juhudi kufuata yote aliyofanya
Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ili tuchume
thawabu nyingi zaidi.
Allah ndie mjuzi zaidi.